WAANDISHI WA HABARI KEMEENI VURUGU NA UDHALILISHAJI KWA WANAWAKE TAMWA ZNZ

WANDISHI  wa Habari  nchini wametakiwa kuwa walinzi wazuri kwa wanawake watakaogombea nafasi mbali mbali za uongozi ili kuripoti na kukemea ukatili dhidi yao katika  kipindi cha Uchaguzi.


Ameyasema hayo, Mkurugenzi wa chama cha wandishi wa Habari wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ ) Dk Mzuri Issa katika mafunzo ya siku moja, yaliyofanyika katika Ofisi ya chama hicho huko Tunguu,na kuwashirikisha wandishi wa vyombo mbali mbali vya Habari.

Dk Mzuri, amesema kuelekea kipindi cha uchaguzi wandishi wa Habari  wana jukumu  kubwa la  kufanya kazi yao ya ulinzi ili kuwalinda wagombea wanawake watakaogombea nafasi  mbali mbali za uongozi dhidi ya vurugu na udhalilishaji unaotokea katika  kipindi hicho.

“ Tuna sheria nyingi  ambazo zinamtaka mwanamke ashiriki katika kugombea nafasi za uongozi  hasa sheria ya vyama vya siasa  ya mwaka 2023 ambayo imeongezwa kifungu cha 10 C  ambacho kinavitaka vyama vya siasa kuwa na sera ya jinsia na madawati  katika vyama vyao” amesema Dk Mzuri.

Aidha amewataka wandishi wa Habari kuendelea kuandika Habari za wanawake waliopata  mafanikio katika nafasi za uongozi ili iwe mfano mzuri kwa wanawake  wanaotia nia ya kugombea nafasi mbali mbali za uongozi katika uchaguzi  mkuu wa mwaka huu.

“ Tunao wanawake wengi waliofanya vizuri katika nafasi za uongozi  na wakaleta maendeleo na mabadiliko ya kisiasa lakini pia katika mashirika na makampuni mbali mbali ni vizuri tukawaandikia Makala ili jamii iwajuwe” amesema.


 Nae, Afisa Khairat Haji kutoka TAMWA ZNZ, amesema ni vyema wandishi wa Habari kuelewa pia udhalilishaji unaofanyika katika mitandao ya kijamii na kuweza kukemea .

Amesema kuwa, imezoeleka katika mitandao mbali mbali ya kijamii mwanamke akiweka kitu mfano, picha yake basi watu hawaangalii kile alichokiweka wataanza kumzodoa yeye na muonekano wake na huo pia ni udhalilishaji wa kimtandao.
 Nao baadhi ya Wandishi wa Habari waliopata mafunzo hayo , Berema Suleiman kutoka Zenji FM na Huwaida Nassor wamesema mafunzo hayo, yamewasaidia kuelewa kwa upana umuhimu wa wandishi katika kuwalinda wanawake kipindi cha uchaguzi.

 Wandishi hao, wameahidi wataendelea kuwaelimisha wanawake kutumia haki yao ya msingi ya kuchagua na kuchaguliwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili kuongeza ushiriki wao katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi.

Mafunzo hayo , maalum ya siku moja yameandaliwa na Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ) kwa kushirikiana na Chuo kikuu cha Dar es salaam (UDSM) yamewashirikisha wandishi wa habari 30 wa Zanzibar kwa lengo la kuripoti na kukemea ukatili wa wanawake kipindi cha uchaguzi.


Post a Comment

0 Comments